Wednesday 22 November 2017

SERIKALI YAIPA ONYO TANESCO


Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amewaagiza watendaji wa Tanesco kuhakikisha kuwa hawakati Umeme bila sababu maalum na hivyo kuwaondolea wananchi adha ya kukosa nishati hiyo.

Naibu Waziri aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kukagua mradi wa TEDAP unaohusu upanuzi na ujenzi wa vituo vya kupozea Umeme na njia za Umeme ambapo vituo vya kupozea Umeme alivyovitembelea ni Mbagala, Gongo la Mboto, Kipawa na City Centre.

“Umeme ukatike pale inapostahili tu, na endapo tatizo linatokea mfano kwenye mifumo ya Umeme ni muhimu mkatoa taarifa mapema kwa wananchi,” alisema Subira Mgalu.

Aliongeza kuwa ukatikaji wa Umeme unasababisha malalamiko kutoka kwa Wananchi kwani kukosekana kwa nishati hiyo kunaathiri shughuli nyingi hasa za kimaendeleo na kiuchumi zinazowaingizia kipato.

Aidha Naibu Waziri aliwaagiza watendaji wa TANESCO wanaosimamia mradi huo wa TEDAP jijini Dar es Salaam, kuhakikisha kuwa kazi hiyo inakamilika tarehe 15 Desemba, 2017.

Vilevile alieleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unaendelea vizuri na kwamba kukamilika kwake kutaboresha hali ya upatikanaji wa Umeme katika jiji la Dar es Salaam.

Nawaomba watanzania wawe na matumaini na Serikali ya Awamu ya Tano kwani inajitahidi katika Ujenzi wa miundombinu ya Umeme, nia ikiwa ni nishati ya Umeme kupatikana muda wote,” alisema Naibu Waziri.

kwa upande wake, Meneja Mradi wa Usafirishaji na Usambazaji Umeme kutoka TANESCO, Mhandisi Emmanuel Manirabona alisema kuwa Shirika hilo linafanya juhudi mbalimbali ili utekelezaji wa mradi huo ukamilike ndani ya muda ulioelekezwa.

Mradi wa TEDAP unahusisha upanuzi na ujenzi wa Vituo Vipya 19 vya kupoza Umeme wa Msongo wa kV 132/33 na kV 33/11 pamoja na ujenzi wa njia za Umeme wenye Msongo wa kV 132, kV 33 na kV 11 katika Mikoa ya Arusha, Dar es Salaam na Kilimanjaro.


Gharama za utekelezaji wa mradi husika ni Dola za Marekani milioni 43, ambazo zimetolewa na Benki ya Dunia (WB) kupitia Mradi huo.

No comments:

Post a Comment