Sunday 5 November 2017

PROF. MBARAWA AWATAKA WAKAZI WA GEITA KUTUMIA VIZURI FURSA ZA UJENZI WA UWANJA WA NDEGE

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akisalimia wananchi wakati wa sherehe za uwekaji wa jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa ndege wa mkoa wa Geita unaojengwa wilayani humo kwenye sherehe zilizofanyika leo Jumamosi Novemba 4, 2017. Uwanja huo ambao utakuwa na njia yenye urefu wa kilomita 3, unajengwa na makandarasi wazalendo.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, amewataka wananchi wa mkoa wa Geita kutumia fursa ya ujenzi wa Uwanja wa ndege wa kisasa wa Geita kujikomboa kiuchumi.
Profesa Mbarawa aliyasema hayo mapema leo  wakati alipokuwa akiweka jiwe la msingi la uwanja huo katika kijiji cha Nyabilezi mkoani Geita na kusisistiza kila mwananchi kuangalia namna atakavyonufaika na uwanja huo.  

“Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba usafiri wa anga unaimarika ili kurahisisha huduma ya usafirishaji wa abiria, hivyo kuvutia watalii katika vivutio mbalimbali nchini”, amesema Profesa Mbarawa.

Aidha, Profesa Mbarawa, amewataka wakazi wa Kanda ya Ziwa, kutumia fursa ya uwepo wa Uwanja wa ndege huo kukuza utalii, kilimo, ufugaji na biashara ya madini ili kuhuisha uchumi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Waziri Mbarawa aliongeza kuwa katika kuhakikisha Usafiri wa anga nchini unaimarika Serikali  imekarabati Viwanja vya ndege vya Mpanda, Bukoba, Tabora na Mafia na ina mpango wa kuvijenga kwa kiwango cha kisasa viwanja 11 nchini ili kuwezesha ndege mpya za Shirika la Ndege  (ATCL), kutoa huduma katika mikoa mbalimbali.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Mhandisi Patrick Mfugale, alisema ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa mkoa wa Geita ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya usafiri wa anga nchini ya mwaka 2003 inayooelekeza uwepo wa uwanja wa ndege wa kisasa katika kila mkoa ili kurahisisha uchukuzi na kuchochea fursa za kibiashara na kitalii katika maeneo mbalimabali ya nchi.

Mhandisi Mfugale, aliongeza kuwa Uwanja wa Ndege wa Geita ambao unajengwa na Kampuni ya kikandarasi ya Mayanga ambayo ni ya mzawa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi Bilioni 41.

“Uwanja huu utakapokamilika utawezesha ndege kubwa aina ya Boeing 737 – 800 zenye uwezo wa kubeba abiria 100 hadi 200  kuruka na kutua, hivyo kuongeza na kurahisisha huduma ya usafiri wa anga katika Ukanda huo”, amesema Mhandisi Mfugale.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Luhumbi, alisema wamejipanga kutumia uwanja wa ndege wa Geita katika kukuza utalii na biashara mkoani humo na kuahidi kuulinda uwanja huo na kutunza miundombinu yake.

Uwanja wa Ndege wa Geita wenye urefu wa Kilometa 3 na upana wa Meta 45 unatazamiwa kuwa na uwezo wa kuegesha ndege kubwa Tatu kwa wakati mmoja pindi utakapokamilika.


No comments:

Post a Comment