Monday 6 November 2017

RAIS MAGUFULI AMERUDISHA NCHI KWA WANANCHI



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amerejesha nchi kwa wananchi na kwamba hayo ni mapinduzi ya ajabu ambayo hayajawahi kutokea katika nchi zetu hususan Afrika.
Maneno hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) Dkt. Ayub Rioba alipofanya mahojiano na redio Uhuru mwishoni mwa wiki iliyopita katika ofisi zao zilizopo Mtaa wa Lumumba jijini Dar-es-salaam.

Dkt.Rioba amesema Mhe. Rais ameirudisha nchi kwa wananchi kwa kuwa anatekeleza “kile anachoambiwa na wananchi, na ahadi alizowaahidi wakati akiwaomba kura” anaeleza Dkt. Rioba na kuongeza kuwa yeye binafsi anamshukuru Mhe. Rais kwa “kuirudishia heshima Tanzania“.

Katika mahojiano hayo, Dkt. Rioba alieleza kuwa tangu kushika madaraka miaka miwili sasa  Rais Magufuli amekuwa ‘busy’ kuhakikisha nchi inakaa sawa kimfumo ndio maana hajashughulika sana na safari za kwenda nje ya nchi.

Rais anataka kutengeneza “mfumo wa kimkataba au kibiashara na hawa mabwana wakubwa (wawekezaji toka nje) utakaowezesha kugawana nusu kwa nusu katika kile kinachopatikana katika uendelezaji wa rasilimali zetu badala ya mifumo ya zamani ya kukubali kila mfumo unaoletwa na nchi zilizoendelea” alisema Dkt. Rioba.

Mkurugezi Mkuu huyo alikieleza kituo hicho cha redio kuwa yeye binafsi anadhani kilichosababisha Kampuni ya kuchimba Dhahabu ya Barrick kumsikiliza Mhe Rais ni umakini wa kiongozi huyo kwa “hanunuliki, hahongwi hongwi maana Afrika ina viongozi wengi ambao wananunuliwa na kuhongwa” lakini sasa wanajua huyu ni tofauti.

Dkt. Rioba anamuona Rais Magufuli kuwa kiongozi anayesimamia mambo yanayo wanufaisha wananchi wake na “hakimbii kimbii kwenda huku na kule kuomba" na kuifananisha nchi yetu na zile zinazotoa misaada katika nchi nyingine. Kwa kuwa fedha wanazozipata zinatokana na  rasilimali zetu na kueendeleza nchi zao.

Mhe Magufuli alisema; “Nchi yetu ilitakiwa kuwa Donor Country, yaani nchi inayotoa misaada kwa nchi nyingine”.

Ninachoweza kuwaambia Watanzania wenzangu miaka miwili ya Serikali ya Awamu ya Tano madarakani, hakika viongozi wetu wameonesha nia nzuri na wanatakiwa kuunga mkono kwa hili analolifanya Rais Magufuli wakati huu wa mpito.

Nchi yoyote inapopita katika mpito ni lazima kuna mambo yalikuwa hayaendi sawa   na mengine yamekwenda sawa. Mpito ukitokea kuna mabadiliko yatakayojitokeza. Mfano Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alipendekeza mfumo wa vyama vingi japo wananchi wengi, bado waliutaka mfumo wa chama kimoja.  Aidha kutokana na kubadilishana uongozi hapa Tanzania, mabadiliko mengi yalijitokeza ambayo yalikuwa mazuri na mengine sio mazuri kwa kuwa ni kipindi cha mpito.

Dkt. Rioba amesema ujio wa Rais Magufuli ulikuwa ujio muhimu sana kwa wakati huu, kwa ajili ya kurekebisha yale yote yaliyojitokeza ambayo hayakuwa sawa. Akitoa mfano wa mwana falsafa mmoja anayeitwa Fans Fanon wakati wa vita vya ukombozi nchini Algeria alisema:
“Kila kizazi kinakutana na majukumu yake ya msingi ya kutekeleza au kuyatelekeza na kusubiri matokeo yake”

Mkurugezi Mkuu huyo wa TBC alieleza kuwa kwa maoni yake Rais Magufuli amekuwa kiongozi sahihi aliyekuja kwa wakati sahihi, ili kurekebisha mambo kwa namna moja au nyingine ambapo hapa na pale tulijikwaa kwa sababu tulitoka nje  ya  misingi iliyojengwa na Taifa letu.

Kuhusu suala la kuwa na uchumi mzuri katika nchi Rioba amesema tafiti zinafanyika kwa mrengo wa kimagharibi zaidi ambapo, wanahalalisha mifumo ya uchumi wanayoitaka wao. Wachumi walio wengi wanasema ili uchumi uwe mzuri na nchi kuendelea ni lazima kuwa na Ardhi, tekinolojia, rasilimali ziwe nyingi nk , lakini sio kweli.

Mfano nchi ya Singapore hawana rasilimali zaidi ya bahari na samaki lakini uchumi wao ni mzuri sababu moja kubwa ni uongozi bora ambao unasimamia matumizi sahihi ya rasilimali kwa manufaa ya wananchi wa nchi husika. Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni nchi ya 4 duniani kwa wingi wa madini lakini haijaendelea, mpaka leo kuna watu wanaomiliki madini katika nchi hiyo wako nje hivyo faida yote inayopatikana kutokana na madini hayo inazinufaisha nchi za nje.

Jambo la msingi Rais Magufuli anataka rasilimali zilizopo, hata kama kidogo kitumike kwa manufaa ya wananchi wanyonge wa Tanzania.  Tanzania ya Rais Magufuli amesema hapana haya madini yanayopatikana hapa Tanzania ni lazima tugawane nusu kwa nusu.

Dkt. Rioba anasema Rais ameonesha mfano kwa nchi nyingine za Afrika zenye rasilimali kama zetu, kuwa hili la kugawana faida nusu kwa nusu, hata kama hatuna tekinolojia na mitaji linawezekana.
Zipo nchi nyingi za Afrika ambazo zilitumia rasilimali zao vibaya mfano, Siera Leoni, Liberia wakawa wanachimba almasi kwa ajili ya kuendesha vita na kununua silaha kutoka nchi 
zilizoendelea.

  Afrika ifike mahali ioneshe ukomavu na kuacha mambo ya kipumbavu kama hayo ioneshe kuwa Afrika ina watu wanaweza kufikiri na kuweza kugawana rasilimali kama alivyofanya Rais Magufuli.
Ukiangalia nchi ya Nigeria asilimia 80 ya mafuta yanayosafirishwa kwenda nje ni asilimia 1 tu ya mafuta hayo ndio yanarudi Nigeria, lakini Tanzana ya Magufuli amesema hapana

Akitoa mfano Dkt Rioba alisema Baba wa Taifa mara baada ya Uhuru wa Tanganyika, wasomi walikuwa wachache sana wasingeweza kutosheleza katika masuala ya utaalam na kuleta maendeleo kupitia rasilimali tulizonazo.  leo hii nchi yetu imepiga hatua kubwa sana katika suala la taaluma na elimu ambapo hatukuwa na Chuo Kikuu hata kimoja. Leo Tanzania ina vyuo vikuu takriban 50, na wataalamu wako wengi, tunachokosa ni Wataalamu wanaoipenda nchi yao wazalendo wenye nia ya kusukuma gurudumu la maendeleo.

Dkt. Rioba anaeleza kuwa ni vizuri kuwa na waaalam vijana  wenye moyo wa kujituma na uzalendo na kuwa tayari kuwa watumishi wa wananchi  na kusaidia kutimiza ndoto ya Tanzania ya viwanda  na ndivyo anavyotaka Rais Magufuli.

Akizungumzia suala la kuondoa dhana ya kuwa na matabaka ya watu katika Taifa,  Rioba amesema kwa sababu Tanzania iko katika mpito, ambapo ilitoka katika misingi ya Ujamaa na Kujitegemea (Azimio la Arusha) na sasa ni kama kutengeneza Azimio la Arusha jipya lakini katika muktadha wa zama za sasa. Kwa wale watanzania ambao ni wazalendo kabisa kabisa, Dkt. Rioba anasema watakubaliana nae kuwa anayoyafanya Rais Magufuli ni lazima aungwe mkono kwa kuwa anaipeleka nchi panapostahili.

Dkt. Rioba katika mahojiano hayo amesema ni wakati sasa kwa kila Mtanzania kuona uchungu kwa kila aina ya wizi wa rasilimali za nchi na kwamba dhambi kubwa ambayo watanzania wanaweza kuifanya ni kudhani kuwa jukumu la kulinda rasilimali za nchi ni la Rais Magufuli pekee.

“Haijawahi tokea kiongozi yeyote barani Afirika kusema wananchi tumeibiwa mno na mbali zaidi, kutafuta suluhisho la kuibiwa huko. Hongera Rais Magufuli jitihada zako ni ukombozi kwa rasilimali zote Barani Afrika na mwisho wa Bara la Afrika kuwa Shamba la Bibi (akimaanisha kila mtu anakuja kujichukulia na kundoka)” Dkt. Rioba alimazilia mahojiano hayo.  

No comments:

Post a Comment