Tuesday 14 November 2017

SERIKALI YA TANZANIA YAISHUKURU SERIKALI YA CHINA



Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe amemshukuru Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Bibi. Wang Ke kwa kuipatia wizara vitendea kazi vyenye thamani ya  shilingi milioni 133.
Waziri Dkt. Mwakyembe ametoa shukrani hiyo leo Ofisini kwake  Mkoani Dodoma alipokutana na Balozi huyo ambapo waliweka sahihi ya makabidhiano ya vifaa hivyo na kuhaidi kuendelea kuimarisha uhusiano huo uliodumu kwa muda mrefu .

 “Nashukuru sana Balozi kwa kutupatia msaada wa vitendea kazi na tunaahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya nchi hizi mbili kwa manufaa ya taifa na watu wake” amesema Mhe.Dkt. Mwakyembe.

Aidha Waziri Dkt. Mwakyembe ameongeza kuwa tayari kumekuwa na juhudi za wazi zinafofanywa na Ubalozi huo kwa kutoa mafunzo ya kubadilishana utaalam kati ya Tanzania na Jamhuri ya watu wa china kupitia sekta za filamu, habari,michezo na utamaduni.

Pia, Dkt. Mwakyembe alimueleza Balozi huyo kuwa Tanzania imepata nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika wenye lengo ya kuhifadhi kumbukumbu za harakati za kuikomboa Afrika ili kuwa na historia nzuri kwa kizazi kijacho.

“Tayari tumeanza maandalizi ya kuhifadhi historia ya wapigania uhuru ukizingatia Tanzania ilikuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha nchi za Bara la Afrika zinakuwa huru, hii ni hatua kubwa kwetu katika kuimarisha mahusiano baina ya nchi zetu ” amesema Mhe. Dkt. Mwakyembe.

Naye Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Bibi. Wang Ke ameeleza kufurahishwa na ushirikiano ulipo baina ya nchi hizo mbili ikiwemo kujifunza tamaduni za China.

“Nimefurahi kuona idadi kubwa ya watanzania wanaojifunza utamaduni wetu kupitia Chuo kikuu cha Dar es Salaama na Chuo kikuu cha Dodoma, ni hatua nzuri na ya msingi katika kuimarisha mahusiano ya nchi zetu” amesema Balozi Wang Ke.


 Tanzania na Jamhuri ya Watu wa China wamekuwa na ushirikiano wa karibu katika kuleta maendeleo tangu mwaka 1960 ambapo walishirikiana katika ujenzi wa reli ya TAZARA na sasa uhusiano huo umezidi kuimarishwa kupitia sekta za habari,filamu, sanaa na utamaduni.

No comments:

Post a Comment