Waziri Mkuu, Kassim
Majaliwa akizungumza na wafanyakazi na viongozi wa kiwanda cha nguo cha Urafiki
cha jijini Dar es salaam baada ya kukagua kiwanda hicho Juni 1, 2018. Kushoto
ni Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage na kulia ni Kaimu
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam na Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi, Evarest
Ndikilo.
Baadhi ya
wafanyakazi wa kiwanda cha nguo cha Urafiki wakimshangilia Waziri Mkuu, Kassim
Majaliwa wakati alipozungumza nao kiwandani hapo, Juni1, 2018.
Waziri Mkuu ,Kassim
Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Mhandisi Mkuu wa kiwanda cha
nguo cha Urafiki cha jijini Dar es salaam, Khamis Mazugo (kushoto) kuhusu
mitambo ya kiwanda hicho iliyokoma kufanya kazi wakati alipotembelea kiwanda
hicho Juni 1, 2018. Kiwanda hicho kimesimamisha uzalishaji tangu Desemba mwaka
jana.
Waziri Mkuu, Kassim
Majaliwa akipita katika eneo zilipong'olewa mashine za kiwanda cha nguo cha
Urafiki cha jijini Dar es salaam wakati alipotembelea kiwanda hicho Juni 1,
2018. Kiwanda hicho kimesimamisha uzalishaji tangu Desemba mwaka jana
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Naibu
Meneja Mkuu wa kiwanda cha nguo cha Urafiki, Shadrack Nkelebe kuhusu mashine za
kutengeneza nyuzi za pamba wakati alipokitembelea kiwanda hicho, Juni 1,
2018. Kiwanda hicho kimesimamisha uzalishaji tangu Desemba mwaka jana.
Serikali imesema
hairidhiki na ubia unaoendeshwa kwenye Kiwanda cha Nguo cha Urafiki.
Hayo yamesemwa na Waziri
Mkuu Kassim Majaliwa leo jioni (Ijumaa, Juni mosi, 2018) wakati akizungumza na
mamia ya wafanyakazi wa kiwanda hicho mara baada ya kukagua mitambo mbalimbali
kwenye kiwanda hicho.
“Serikali haturidhiki na
ubia huu, na huyu mbia aelewe kwamba Serikali haturidhishwi na ubia huu wala
kinachoendelea hapa kiwandani,” amesema huku akishangiliwa kwa nguvu na
wafanyakazi wa kiwanda hicho.
Waziri Mkuu amemuagiza
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Bw. Charles Mwijage aongoze kikao
baina ya wabia hao na menejimenti ya kiwanda na apewe taarifa hiyo leo saa 12
jioni baada ya kufuturu.
“Ubia wenu hauna tija.
Kwa hiyo wewe Msajili wa Hazina na huyo mwekezaji, nikitoka hapa, mbaki mfanye
kikao na mnipe majibu leo saa 12 jioni. Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Mkuu wa
Mkoa muongoze mjadala huo na nikitoka kufuturu mniambie maazimio yenu, na kama
haiwezekani, mvunje kabisa ubia huo ili tujue hatuna mbia tutafute mbia,”
amesema.
Waziri Mkuu amesema
wabia wakuu wa kiwanda hicho ni Msajili wa Hazina na kampuni ya Changzhou State
owned Textile Assets Operations kutoka China na kwamba Serikali ilipoamua
kukaribisha uwekezaji ilitarajia kupata mtaji, teknolojia na ajira za kutosha
lakini hali ya sasa ni kinyume kabisa.
“Hatuwezi kuvumilia,
tunasema tuna mbia mwenye mtaji, hakuna mtaji; tulisema tunataka mbia mwenye
kuleta teknolojia mpya, hakuna teknolojia; tulisema aendeshe shughuli hii
kukiwa na ajira endelevu, hizo ajira hakuna; halafu tubaki tunamwangalia tu.
Bora atuambie amekwama, aondoke, tutangaze vinginevyo,” amesema.
“Tulikopa mtaji lakini
Tanzania hizo hela hazijaja, tunataka majibu ya fedha hizo; kama fedha
iliyokopwa kwenye Benki ya Exim ya China ingeletwa nchini tungeweza kuziba
mapengo na kusaidia kiwanda kiweze kufanya kazi. Sasa kwa sababu fedha hiyo
haijaja nchini, tunataka maelezo fedha hiyo iko wapi?” amesisitiza.
“Mitambo iliyonunuliwa
na mwekezaji miaka mitano au sita iliyopita haifanyi kazi tangu ilipoletwa
nchini, nataka majibu, je mitambo hii ilinunuliwa ikiwa mizima au vipi; na tena
mmeng’oa mashine kwenye ma-godown matatu, nimeambiwa mlikuwa na nia ya kuleta
mashine mpya, lakini sasa ni miaka mitano, je mashine zile zote zimeenda wapi,
na kama mmeuza ameuziwa nani? Mkae mjadili na leo hii mniletee majibu yote
haya,” amesisitiza.
Waziri Mkuu amesema
kiwanda hicho ni matokeo ya urafiki wa China na Tanzania na kina historia ndefu
na mahusiano ya muda mrefu. “Asiingie mtu akatuharibia, na tunataka mahusiano
yetu na China yaendelee. Amesema baada ya kupokea taarifa hiyo, Serikali itakaa
na Balozi wa China ili itafutwe suluhisho.
Waziri Mkuu amewataka
watumishi wa kiwanda hicho walioko likizo na wale waliopo kazini wawe
wavumilivu wakati Serikali ikiendelea kutafuta dawa ya matatizo yao.
Wakati huohuo, Waziri
Mkuu amemtaka Meneja Rasilmali Watu na Utawala wa kiwanda hicho, Bw. Edwin
Nkwanga aandae orodha ya watumishi wote yenye kuonyesha kila mtumishi analipwa
nini na aifikishe kwake haraka.
“Hapa kuna watu
wanalipwa sh. milioni saba hadi 10 na wengine wanalipwa sh. 120,000. Niletee
orodha yenye kuonyesha jina, cheo na kiwango cha mshahara, lakini pia uonyeshe
anapata stahili zipi, kama ni posho ya nyumba, maji au umeme,” amesema.
Amesema nia ya Serikali
ni kutaka kupanga upya mishahara yao ili waweze kupatikana watumishi wa
kutosha.
Wakati akikagua kiwanda
hicho, Waziri Mkuu alielezwa kwamba kuna mashine 88 ambazo ziling’olewa kwenye
kiwanda hicho na hazijulikani zimepelekwa wapi.
Mapema, akitoa taarifa
fupi ya kiwanda hicho, Naibu Meneja Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Shadrack Nkelebe
alisema kiwanda hicho kimesimamisha uzalishaji tangu Desemba 2017 ili kufanya
ukarabati na kimeshindwa kuendelea nao kwa sababu ya madeni.
“Kiwanda kilikuwa na
watumishi 3,000 lakini sasa hivi wamebakia 726 baada ya wengine kupunguzwa na
kulazimishwa kwenda likizo licha ya teknolojia kubakia ni ileile. Kiwanda
kinakabiliwa na changamoto nyingi lakini kwa sehemu kubwa ni za kutengeneza.
Tumepigana vita katika kujenga uchumi wa Taifa kupitia kiwanda hiki, lakini
tumekwama. Tunahitaji nguvu ya ziada ili tutoke hapa,” alisema
No comments:
Post a Comment