Wednesday 9 March 2016

RAIS WA VIETNAM, MHE. TRUONG TAN SANG AWASILI TANZANIA.



Akipunga mkono na mkewe mara baada ya kuwasili nchini.

Waziri mkuu, Mh. Kassim Majaliwa akimpokea mara baada ya kuwasili jana.

Mh.Truong Tan Sang akishuka kwenye ndenge  na mkewe mara baada ya kuwasili nchini katika uwanja wa J k Nyerere jijini Dar es salaam.

Raisi wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam, Truong Tan Sang, amewasili  nchini  jana  saa  mbili  usiku tayari kwa  kuanza ziara ya siku tatu nchini, ambapo pamoja na masuala mengine, atasaini mkataba wa masuala ya Kodi na mwenyeji wake Rais John Magufuli.


Mkataba huo unalenga kuchochea biashara kati ya Vietnam na Tanzania kwa kuwa utatoa fursa kwa wafanyabiashara wa pande zote kutotozwa kodi mara mbili katika biashara na uwekezaji watakaoufanya.

Rais huyo anatarajiwa kupigiwa mizinga 21 leo, ikiwa ni pamoja na kukagua gwaride rasmi, ambapo baadaye atatambulishwa kwa viogozi mbalimbali wa Serikali, kabla ya kufanya mazungumzo na Rais Magufuli.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa Dar es Salaam kuhusu ujio wa Rais huyo wa Vietnam, baada ya viongozi hao kutia saini mkataba huo, mgeni huyo na ujumbe wake atakwenda kwenye ofisi ndogo ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), iliyopo katika Mtaa wa Lumumba jijini humo kukutana na Mwenyekiti wa chama hicho, ambaye ni Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete.

Rais huyo wa Vietnam ambaye ni mmoja wa viongozi waandamizi wa Chama cha Kikomunisti cha nchi hiyo chenye uhusiano wa muda mrefu na CCM, atakwenda kwenye Mamlaka ya Ukanda Maalumu wa Uwekezaji (EPZA) Ubungo, Dar es Salaam kutembelea viwanda na kupata taarifa za fursa za uwekezaji katika sekta ya viwanda nchini.

Aidha, ratiba hiyo imeeleza kuwa atahudhuria mkutano wa biashara na uwekezaji kati ya nchi hizo mbili, kabla ya kukutana na Spika wa Bunge, Job Ndungai na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein katika wakati tofauti.


Pamoja na ujumbe wake atatembelea hifadhi ya wanyama ya Saadan iliyoko Bagamoyo na kuondona nchini Machi 11 kuelekea Msumbiji kuendelea na ziara yake.

No comments:

Post a Comment