Friday 9 March 2018

CCM WILAYA YA GEITA WAUNGA MKONO UJENZI WA VYUMBA VYA MADARASA

Katibu wa siasa na uenezi wa CCM Wilaya ya Geita,Bw Jonathan Masele pamoja na baadhi ya viongozi wakishiriki kuchimba msingi kwenye shule ya msingi ya Kaseni iliyopo Kata ya Mtakuja.

Viongozi wa chama cha mapinduzi(CCM)wakishiriki kuchimba msingi wa shule ya msingi Kaseni.

Kaimu afisa elimu halmashauri ya mji wa Geita,Mwl Salome Cheleani,akishiriki zoezi la uchimbaji wa msingi wa shule ya msingi Kaseni. 

Mwenyekiti wa CCM wilayani ya Geita ,Barnabas Mapande akishirki zoezi la uchimbaji wa msingi shule ya msingi Kaseni. 

Wananchi wakiwa kwenye zoezi la kuchimba msingi shule ya msingi Kaseni.

Wananchi wakiwa wamesimama mbele ya msingi wa shule ya msingi Kaseni.

Katibu wa siasa na uenezi wa CCM Wilaya ya Geita,Bw Jonathan Masele akizungumza na waandishi wa habari juu ya kujitolea katika shughuli ya ujenzi wa madarasa.

Wananchi wakisomba mawe kwaajili ya ujenzi wa msingi wa shule ya Kaseni.





Halmashauri ya mji wa Geita inakabiliwa na upungufu wa vyumba vya madarasa elfu moja na sabini  na tisa (1,079)  huku mahitaji yakiwa ni elfu moja miatano na saba (1,507) na ambavyo vipo ni mianne ishirini na nane (428) .

Hali hii imewasukuma  viongozi wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilayani Geita,kushirikiana na wananchi kwenye  ujenzi wa vyumba vya madarasa kwenye shule ya msingi Kaseni  iliyopo Kata ya Mtakuja Wilayani humo,lengo likiwa ni kupunguza changamoto ambazo zimeendelea kuwakumba wanafunzi  kusomea nje.


Akizungumza wakati wa shughuli hizo ,Katibu wa siasa na uenezi wa CCM,Bw Jonathan Masele amesema wameamua kufanya hivyo kutokana na ilani ya chama kuelekeza kushiriki katika suala la maendeleo na kwamba kufanya hivyo kutasaidia  kuwaepusha watoto kukaa nje ya madarasa.

“Tumeamua  kwa sababu ilani yetu ya chama cha mapinduzi inaelekeza kutekeleza majukumu ya wananchi kwa kuwasaidia kujenga mashule kufanya kazi za mikono ,hii ilani yetu tunaitekeleza ili kuhakikisha watoto wanasoma kwenye mazingira mazuri” Alisema Masele.

Mwenyekiti wa CCM wilayani humo,Barnabas Mapande amewataka wananchi kujitolea kufanya kazi za maendeleo na kuachana na dhana ya maandamano yasiyokuwa na msingi kwa Taifa ,kwani ni vyema kuendelea kuunga mkono juhudi za Rais za kuboresha miundombinu ya Elimu.

“Tunahitaji kufanya kazi muda wa maneno umekwisha awamu hii ni ya kazi wanaosema maandamano wakaandamane lakini hutakiwi kuandamana kama unataka maandamano kasombe mawe, kuchimba msingi tufanye kazi kwa ajili ya watoto wetu wanaandamana waende huko lakini cha moto watakiona sisi tufanye kazi za maendeleo” Alisisitiza Mapande.

Aidha Kaimu afisa elimu halmashauri ya mji wa Geita,Mwl Salome Cheleani ameelezea kuwa wanaendelea na mikakati ya ujenzi wa madarasa na kuyamalizia maboma ambayo yalikuwa bado hayajakamilika na kwamba wana imani mwaka huu watapunguza kwa kiasi kikubwa mahitaji ya vyumba vya madarasa.

No comments:

Post a Comment