Friday 14 April 2017

WIZARA YA MAJI NA UMWAGILIAJI YATEKELEZA: DAWASA UKINGONI KUKAMILISHA KAZI



Kazi ya ujenzi wa laini mpya ya umeme wenye nguvu ya 33KV kutoka Chalinze (Sub-station) kwenda Mlandizi yenye urefu wa kilomita 45 kwa lengo la kuongeza umeme ili kukidhi mahitaji ya upanuzi wa mtambo uliofanyika na kuweza kusukuma ujazo wa lita za maji milioni 196 kwa siku sasa umekamilika na majaribio ya matumizi ya laini hiyo yameanza kwa matarajio ya kukamilisha kazi hiyo ndani ya siku mbili.
Taarifa ya Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) ilifafanua kwamba, DAWASA kupitia Mkandarasi wake M/s WABAG kutoka nchini India kwa kushirikiana na Mkandarasi Msaidizi, Kampuni ya M/s Mollel Electrical Contractors ya hapa nchini kwa sasa wamemaliza kazi zote za ujenzi wa laini kutoka Chalinze mpaka eneo la kuingizia umeme ndani ya Mtambo wa Maji wa Ruvu Juu uliopo Mlandizi tayari kwa majaribio ya awali ya kiusalama na kuwasha pampu.

Mtambo huo wa maji wa Ruvu Juu utakua ukipokea umeme wa kutosha kutoka katika transfoma kubwa iliyopo kituo kidogo cha umeme Chalinze (Sub-station) yenye uwezo wa 45/55 MVA ambapo itawezesha pampu zote mpya zilizofungwa kuwashwa. 

Hapo awali mtambo huo ulikuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 82 kwa siku na mara baada ya majaribio haya na kuongeza umeme ndani ya siku mbili uzalishaji wake utaongezeka kufikia lita milioni 196 kwa siku.

Taarifa ya DAWASA inabainisha kuwa, ili lita hizo milioni 196 za maji ziweze kusukumwa na mtambo huo wa Ruvu Juu, mtambo unahitaji 16MVA za umeme ili kusukuma maji safi yanayozalishwa baada ya upanuzi kwa asilimia100. 

Aidha, Mkandarasi kwa sasa amekamilisha kazi ya kujenga laini hiyo mpya toka sub-station ya Chalinze ikiwa ni pamoja na kazi zote zilizotakiwa kufanyika ndani ya kituo hicho kidogo cha umeme cha Chalinze. Hizo ni pamoja na kazi mbalimbali zilizotakiwa kufanyika ili kuweza kuupokea umeme huo kutoka kwenye transfoma hiyo.

Aidha, maeneo nufaika ya mtambo wa maji wa Ruvu Juu ni Mkoa wa Dar es Salaam, mkoa wa Pwani, maeneo ya mji wa Mlandizi, Kibaha na baadhi ya Vitongoji vyake.

DAWASA inaendelea kulishukuru Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa ushirikiano na ushauri wa kitaalam kuhusiana na masuala ya umeme ambao imekua ikiutoa mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa maji ya kutosha yanapatikana katika jiji la Dar es Salaam na maeneo yote yanayohudumiwa na DAWASA.


Mikataba ya upanuzi wa mtambo na ujenzi wa mabomba mapya kutoka Ruvu Juu mpaka Kimara pamoja na ujenzi wa tanki kubwa lenye ujazo wa lita million 10 ilisainiwa mwaka 2014 na Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji ilipata fedha hizo kwa mkopo wa masharti nafuu toka Benki ya Exim ya India.

No comments:

Post a Comment