Wednesday 10 August 2016

KIFUKWE AMTAKA MANJI ALETE MAOMBI YAKE KWA MAANDISHI



Kifukwe amemtaka Manji awasilishe mapendekezo yake ya kutaka kuikodisha klabu kwa maandishi

MJUMBE wa Baraza la Wadhamini la Yanga, Francis Mponjoli Kifukwe amemtaka Mwenyekiti wa klabu, Yussuf Manji anayetaka kuikodisha klabu kwa miaka 10 kuwasilisha mapendekezo yake kwa maandishi.

Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Kifukwe alisema kwamba baada ya Mkutano wa Jumamosi, alimuambia mfanyabiashara huyo awasilishe maombi yake kwa maandishi.
“Tunasubiri mapendekezo yake rasmi katika maandishi, ili sisi (Baraza la Wadhamini) tuanze kuyafanyia kazi,”alisema Kifukwe jana.

Hii inamaanisha pamoja na wanachama wa Yanga kukubali kubadilisha mfumo wa kuiendesha klabu huyo na kuafiki kuimilikisha kwa mtu mmoja, lakini watalazimika kusubiri taratibu zifuatwe. 


Katika mkutano mkuu wa dharula uliofanyika Jumamosi ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam, wanachama wa Yanga walikubali kumkodisha klabu Mwenyekiti wao kwa miaka 10.

Hiyo ilifuatia Manji kutoa pendekezo la kukodisha klabu kwa miaka 10 amilikishwe nembo na timu na katika kipindi hicho atakuwa anachukua asilimia 75 ya mapato ya timu, huku asilimia 25 ikibaki kwa wanachama.

Siku hiyo katika mkutanuo huo, wanachama watatu wa klabu hiyo, Ayoub Nyenzi, Salum Mkemi na Hashim Abdallah walifukuzwa, wakati mmoja, Siza Lyimo alinusurika baada ya kuomba msamaha na kusamehewa.


No comments:

Post a Comment