Monday 29 February 2016

MAHAKAMA YA MAFISADI KUANZA KUFANYA KAZI


Mwanasheria  mkuu wa serikali, George Masaju amesema mahakama maalumu ya mafisadi inasukwa na itatekelezwa kwa muundo wa mahakama, ikiwa ni kitengo ndani ya Mahakama Kuu.

Masaju alisema Muswada wa Sheria ya kuanzisha Mahakama Maalumu ya Mafisadi uko tayari na utawasilishwa Aprili mwaka huu bungeni, kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa kuwa sheria, kutoa nafasi kwa mahakama hiyo kuanza kazi.
“Mahakama ya mafisadi na wala rushwa ipo, tunaisuka na itatekelezwa kwa muundo wa mahakama zetu, itakuwa ni kitengo maalumu ndani ya Mahakama Kuu, kinachoshughulika na masuala ya ufisadi na rushwa,” alisema Masaju.
Akizungumza mwishoni mwa wiki iliyopita, usiku, kwenye kipindi cha Siku 100 za Serikali ya Awamu ya Tano kinachorushwa na Kituo cha Utangazaji cha Taifa cha TBC1, Mwanasheria huyo alisema mchakato wa uanzishwaji wake uko kwenye hatua nzuri kabla ya kuwasilishwa kwenye mkutano wa Bunge ujao.
Alisema ana imani wabunge wote wataunga mkono muswada huo kwa kuwa ni suala la Watanzania.
Akizungumza kwenye mkutano wa pili wa Bunge la 11, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Harrison Mwakyembe alisema wizara yake imeanza maandalizi ya muswada huo wa kuanzisha Mahakama Maalumu ya mafisadi.
Dk Mwakyembe alisema wanafanyia kazi suala hilo kwani ahadi iliyotolewa na Rais lazima ifanyiwe kazi na ufumbuzi uwepo. Aidha Mwakyembe alisema wananchi wavute subira kwa sababu mambo mazuri hayahitaji haraka na mchakato wake ukikamilika watajulishwa.
Rais John Magufuli alipohutubia wakati wa ufunguzi wa Bunge, Novemba 20,mwaka jana, aliendelea kusisitiza mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi akisisitiza juu ya azma ya kuanzisha mahakama hiyo.
Alisema vitendo vya rushwa na ufisadi vyenye madhara makubwa kwa nchi na ustawi wa nchi, hutendwa na watu wenye dhamana kubwa za uongozi na utumishi, ambazo wamezipata kutokana na ridhaa ya watu.

Katika kushughulikia tatizo hilo, aliahidi kuunda Mahakama ya Rushwa na Ufisadi na kusema ana matumaini vyombo husika havitamkwamisha.

No comments:

Post a Comment