Saturday 18 June 2016

SERIKALI YAPOKEA MSAADA WA MAGETI 27 KWA AJILI YA UWANJA WA TAIFA











 Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura akisalimiana na Kaimu Meneja wa Uwanja wa Taifa Bw. Julius Mgaya Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Taifa kupokea msaada wa mageti 27 kutoka kampuni ya TING yenye thamani ya Sh. Million 44 kwa ajili ya kuweka vizuizi kulinda uharibifu wa miundombimu uwanjani hapo.


Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura akisalimiana na Mkurugenzi wa Kampuni ya Ting Dkt Vernon Fernandes mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Taifa kupokea msaada wa mageti 27 kutoka kampui ya TING yenye thamani ya Sh. Million 44 kwa ajili ya kuweka vizuizi kulinda uharibifu wa miundombimu uwanjani hapo.


Muonekano wa Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam wenye uwezo wa kuingia watu 60,000 waliokaa.

Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imepokea jumla ya mageti 27 kutoka Kampuni ya Ving’amuzi ya TING vyenye thamani ya Sh. Million 44.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Anastazia Wambura ameushukuru Uongozi wa Kampuni ya TING kwa msaada mkubwa wa mageti walioupata kwani utasaidia kutatua changamoto ya kukosa vizuizi vya mageti katika Uwanja wa Taifa, ambapo kabla ilikuwa ikisababisha vifaa vingi kuibiwa uwanjani hapo.

“Serikali na Wizara yetu kwa ujumla inaishukuru sana kampuni yako kwa moyo wa utu na kujitolea kwa manufaa ya Watanzania na wapenda michezo kwa ujumla” Alisema Mhe. Wambura.

Aliongeza kuwa, mara baada ya kufungwa kwa vizuizi hivyo vya mageti katika uwanja huo, marekebisho ya miundombinu iliyoharibiwa yatafanyika ili kurudisha hali ya usalama kwa miundombinu hiyo.
Aidha, amewaomba wadau wa michezo nchini kuiga mfano wa kampuni ya TING kwa kushirikiana na Serikali katika kuboresha shughuli mbalimbali za michezo ili kuwezesha watanzania kupata huduma bora na kuendeleza Michezo nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Ting, Dkt. Vernon Fernandes ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kukubali kushirikiana nao katika kuboresha na kuendeleza sekta ya michezo nchini.


Msaada huo wa mageti 27 kutoka katika kampuni hiyo umekuja mara baada ya Naibu Waziri wa habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Mhe. Anastazia Wambura kutembelea uwanja wa Taifa mapema mwaka huu na kujionea uharibifu wa miundombinu ambapo kampuni ya Ting iliahidi kutoa mageti 26 kati ya 42 yanayohitajika.

No comments:

Post a Comment