Saturday 9 April 2016

WACHINA KIZIMBANI KWA TUHUMA ZA KUKWEPA KULIPA KODI


Raia wawili wa China, Ma Jun na Huifang Ma leo wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala kujibu mashtaka mawili likiwamo la kushindwa kutumia  Mashine ya Kodi za Kielektroniki (EFDs) katika biashara zao.


Jun na Ma, ambao wote ni  wafanyabiashara na wakazi wa Mtaa wa Narung’ombe eneo la Kariakoo wanakabiliwa na kushindwa kutumia mashine za EFDs pamoja na kushindwa kujisajili katika kodi ya ongezeko la Thamani(Vat) wakati wakijua kufanya hivyo kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.

Hata hivyo, mshtakiwa wa kwanza katika kesi hiyo, Jun hakuwepo mahakamani hapo kwa madai kuwa yupo nje ya nchi na upande wa mashtaka umeiomba Mahakama kutoa hati kwa ajili ya kumkamata mshtakiwa huyo.

Akisoma hati ya mashtaka, mbele ya Hakimu Mkazi Mwanadamizi Mfawidhi wa mahakama hiyo Said Mkasiwa, Wakili kutoka Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), Cherubin Chuwa alidai kuwa washtakiwa kwa pamoja walitenda  makossa hayo Machi 23,mwaka huu.

Chuwa alidai siku hiyo ya tukio, washtakiwa hao ambao wanamiliki Kampuni ya HM Textile  Co Ltd  Iliyopo  block 54 katika kiwanja namba 6 kilichopo mtaa wa Agrey  eneo la Kariakoo, walishindwa kutumia  mashine za EFDs kwa ajili ya kutoa risiti kwa wateja wao ambao walikuwa wanafanya manunuzi mbalimbali katika duka hilo ambalo linauza mapazia na nguo mbalimbali, huku wakijua kuwa ni kosa kisheria.

Mwandesha Mashtaka huyo aliendelea kudai kuwa, katika shitaka la pili ambalo pia linawakabili washtakiwa wote, inadaiwa kuwa muda na siku hiyo  hiyo katika duka hilo, washtakiwa walishindwa kujisajili katika kodi ya ongezeko la Thamani(Vat) wakati wakijua kufanya hivyo kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.

Chuwa alidai washtakiwa hao walishindwa kujisajili katika Kodi ya Ongezeko la Thamani(Vat) ambayo ni kinyume cha sheria , na kwamba mashtaka hayo yamefunguliwa kupitia sheria za TRA.

Hata hivyo mshtakiwa wa  pili, Huifang  alikiri shtaka la kwanza huku shtaka la pili akikana kuhusika.
Kutokana na hatua hiyo wakili Chuwa alisema dhamana ya mshtakiwa huyo iko wazi ambayo ni kuwa na wadhamini wawili kila kutoka taasisi inayotambuliwa kisheria watasaini bondi ya Sh 3milioni na kuwasilisha mahakamani hati yake ya kusafiria.

Mshtakiwa huyo alishindwa kutimiza masharti ya dhamana na kurudishwa rumande hadi April 21, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment