Thursday 7 April 2016

TAREHE 7 APRIL RWANDA INAADHIMISHA KUMBUKUMBU YA MAUAJI YA KIMBARI YALIYOTOKEA MWAKA 1994



Siku ya leo April 7, Rwanda inaadhimisha miaka 22 ya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari yaliyotokea nchini humo mwaka 1994. Watu zaidi ya laki nane kutoka jamii ya Watutsi ikiwa ni pamoja na Wahutu wa msimamo wa wastani waliokua hawakubaliani na itikadi za Wahutu wenye msimamo mkali hasa chama cha MRND waliuawa.
Chama cha MRND kilikua chama tawala wakati huo, kikiwa na wanamgambo waliojulikana kwa jina la INTERAHAMWE ambao walihusika katika mauaji hayo.
Mauaji hayo yalitokea baada ya kifo cha rais Juvenal Habyarimana, ambaye alikua aliambatana na mwenzake wa Burundi, Cyprien Ntaryamira, usiku wa tarehe 6 kuamkia 7 Aprili mwaka 1994.

Karibu shughuli zote zimesimama kwa siku ya leo, ambapo inaaaza wiki ya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari. Siku hii ni muhimu kwa Wanyarwanda walio ndani na nje ya nchi hasa wale ambao walipoteza ndugu na jamaa zao.

Sherehe rasmi zitaanza saa tano saa (11:00) saa za Afrika ya Kati sawa na saa sita saa za Afrika ya Mashariki. Baa zote zimepigwa marufuku kufungua kwa siku ya leo. Kupiga muziki ndani ya gari au ndani ya nyumba pia imepigwa marufuku.

Viongozi mbalimbali kutoka ukanda huu watahudhuria sherehe hizi. Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli anafanya ziara ya siku mbili nchini humo kuanzia Jumatano hii Aprili 6. Hii ni ziara ya kwanza ya Rais Magufuli nje ya nchi tangu alipochukua hatamu ya uongozi wa nchi mwezi Oktoba mwaka jana.
"Nimetekeleza mwaliko wa ndugu yangu Kagame”
Rais Magufuli amesema alialikwa kutembelea nchi nyingi, lakini hajafanya hivyo akibaini kwamba ni kutokana na sera yake ya "kubana matumizi".
''Nimealikwa kutembelea nchi nyingi, bado sijafanya hivyo. Lakini nilipoalikwa na ndugu yangu Rais Kagame tayari nimetekeleza hilo, na ndo maana nipo hapa, '' amesema Rais Magufuli.

Alhamisi hii, Aprili 7, Rais Magufuli ataungana na wananchi wa Rwanda katika maadhimisho ya miaka 22 ya kumbukumbu ya mauaji ya kimbari na baadaye atakutana na wandishi wa habari akiwa pamoja na Rais Paul Kagame.
Ifahamike kwamba Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli na mwenyeji wake Paul Kagame, Jumatano hii, wamefanya uzinduzi wa daraja la Rusumo linalounganisha Tanzania na Rwanda.

No comments:

Post a Comment