Monday 25 April 2016

ASKARI WANNE WANAODAIWA KUMPIGA MVUVI WAANZA KUCHUNGUZWA NA JESHI LA POLISI MKOANI KAGERA.

Askari Polisi wanne kutoka wilaya ya Muleba mkoani Kagera, wanachunguzwa na Jeshi la Polisi mkoani Mwanza kwa tuhuma za kumpiga na kumjeruhi mvuvi mmoja wa kisiwa cha Kunene wilayani Ukerewe Tabibu Kilangi kwa tuhuma za wizi wa injini za mitumbwi zinazodaiwa kupatikana kwa njia ya unyang’anyi wa kutumia silaha.

Mvuvi huyo ambaye kwa hivi sasa amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi katika hospitali ya rufaa Bugando jijini Mwanza,akiwa amepoteza fahamu huku akipumulia mashine kwa siku ya tano mfululizo anadaiwa kupigwa na askari polisi wa wilaya ya Muleba Aprili 15 mwaka huu katika kisiwa cha Siza kwa kumtuhumu kuiba injini za mitumbwi ya wavuvi wenzake.

Baadhi ya ndugu wa majeruhi,Yohana Wakori na Pendo Charles wakizungumzia tukio hilo wameiomba serikali kutenda haki ikiwemo kuwachukulia hatua za kisheria askari polisi hao wanaodaiwa kuhusika na vitendo hivyo vya kikatili.

Daktari bingwa wa kitengo cha wagonjwa mahtuti katika hospitali ya rufaa Bugando Dk. Benard Kenemo anasema maendeleo ya kiafya ya majeruhi huyo bado hayaridhishi,huku Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Augustine Senga akizungumza na ITV kwa njia ya simu kutokea wilayani Magu amesema jeshi la polisi bado linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.

No comments:

Post a Comment