Tuesday 24 May 2016

SERIKALI IMEDHAMIRIA KUIFANYA TANZANIA KUWA NCHI YENYE UCHUMI WA KATI KWA KUBORESHA MAZINGIRA YA BIASHARA



Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera,Uratibu,Bunge,kazi,Ajira na watu wenye ulemavu Dkt. Hamis Mwinyimvua(Kushoto) akizungumza wakati wa akifungua mkutano wa wadau wa biashara nchini uliolenga kujadili namna ya kuboresha mazingira ya biashara katikati ni Mkurugenzi Mtendaji  wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania Godfrey Simbeye na kulia ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara(TNBC) Raymond Mbilinyi.



Mkurugenzi Mtendaji  wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania Godfrey Simbeye(Katikati) akichangia hoja katika mkutano wa wadau wa biashara nchini uliolenga kujadili namna ya kuboresha mazingira ya biashara kushoto ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera,Uratibu,Bunge,kazi,Ajira na watu wenye ulemavu Dkt. Hamis Mwinyimvua na kulia ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara(TNBC) Raymond Mbilinyi.



Wadau wa biashara kutoka sekta za umma na binafsi wakifatilia mkutano uliofanyika leo uliolenga kujadili namna ya kuboresha mazingira ya biashara nchini.

Serikali imedhamiria kuboresha mazingira ya biashara nchini ili kuongeza uwekezaji na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa Kati.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es salaam na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera,Uratibu,Bunge,kazi,Ajira na watu wenye ulemavu Dkt. Hamis Mwinyimvua wakati akifungua mkutano wa wadau wa biashara nchini uliolenga kujadili namna ya kuboresha mazingira ya biashara.

Dkt. Hamis Mwinyimvua amesema Serikali imeazimia kuboresha mazingira ya biashara nchini kwa kuandaa sera ambazo zitawasaidia wafanyabishara kuwekeza katika sekta mbalimbali.  

“Tutahakikisha tunaboresha mazingira ya biashara kwani hakuna uwekezaji utakaowezekana kama mazingira ya ufanyaji wa biashara yatakuwa hayaridhishi.” Alisisitiza Dkt Mwinyimvua.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara(TNBC) Raymond Mbilinyi amesema kuwa kuna haja ya Taasisi zote za umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja ili kuboresha mazingira ya biashara.

Naye Mkurugenzi Mtendaji  wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania Godfrey Simbeye amesema kuwa Serikali ya awamu ya tano imeanza kufanya maboresho katika mazingira ya uwekezaji.

Akifafanua kuhusu maboresho hayo Simbeye alisema kwasasa ujasili wa makampuni unafanyika kwa kutumia mfumo wa kieletroniki ambapo muombaji anaweza kusajili kampuni pasipo kufika katika Ofisi za BRELA katika kipindi cha muda mfupi.

Mkutano huu uliondaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu ikishirikiana na Baraza la Taifa la Biashara, Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania wakishirikiana na taasisi za umma na binafsi umedhamiria kuwezesha wafanyabiashara na wawekezaji kuwa mazingira mazuri ya kufanya biashara.


No comments:

Post a Comment