Tuesday 20 September 2016

TIMU YA SOKA YA WANAWAKE(KILIMANJARO QEENS) WATWAA KOMBE LA CECAFA CHALLENGE



Timu ya soka ya wanawake ya Tanzania Bara (The Kilimanjaro Qeens) imetwaa kombe la Challenji kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, baada ya kuifunga Kenya, mabao 2-1 katika mchezo wa fainali uliopigwa leo Jinja , nchini Uganda.
Kwa matokeo hayo, Kilimanjaro Qeens wanakuwa ndiyo mabingwa wa kwanza na wa kihistoria wa michuano hiyo ambayo ni mipya kabisa kuanzishwa katika ukanda ukanda wa Afrika Mashariki chini ya baraza lake la CECAFA.
Mabao ya timu ya taifa Tanzania ya wanawake maarufu kama Kilimanjaro Queens katika mchezo wa leo Septemba 20, 2016 yamefungwa na Mwanahamisi Omari katika kipindi cha kwanza kabla ya Kenya kujitutumua na kupata bao la kufutia machozi kipindi cha pili katika mchezo uliokuwa na ushindani wa aina yake.

Kilimanjaro Queens iliingia fainali baada ya ushindi wa 4-1 dhidi ya wenyeji, Uganda, wakati Kenya iliifunga 3-2 Ethiopia ambapo Tanzania Bara iliongoza Kundi B baada ya kushinda kura ya sarafu kufuatia sare ya 0-0 na Ethiopia katika mchezo wa mwisho wa kundi hilo, hivyo kufungana nayo kwa pointi na wasatani wa mabao kileleni.

Kilimanjaro Queens ilianza vizuri michuano hiyo kwa kuibamiza 3-2 Rwanda, mabao yake yakifungwa na Asha Rashid ‘Mwalala’ dakika za 11 na 65 na Stumai Abdallah dakika ya 28, wakati ya wapinzani wao yalifungwa na Ibangarrue Marie na Amina Ally wa Tanzania Bara aliyejifunga.

Afisa habari wa Shirikisho la Soka Tanzania TFF, Alfred Lucas, amesema timu hiyo inaondoka Uganda leo, na itapitia mkoani Kagera ambako itakaa kwa siku moja kwa ajili ya kuwafariji waathirika wa tetemeko la ardhi, na kisha kesho kutwa itawasili jijini Dar es Salaam, ikiwa na kombe lake, na kwamba utaratibu wa mapokezi unaandaliwa.

Kwa niaba ya TFF, Lucas ameipongeza timu hiyo, na kuwaahidi wapenzi wa soka nchini makubwa zaidi.

No comments:

Post a Comment