Tuesday 20 February 2018

WATOTO WA KIKE MUWE CHACHU YA MAPAMBANO DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA HASA MIMBA NA NDOA ZA UTOTONI: DKT NDUGULILE



 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt Faustine Ndugulile


Watoto wa kike nchini wameaswa kujitambua, kujiamini na kujilinda dhidi ya vishawishi vinavyosababisha matukio maovu ya Ukatili wa Kijinsia zikiwemo mimba na ndoa za utotoni na kusababisha kukatisha ndoto zao za kupata haki ya kuendelezwa na elimu bora kwa manufaa yao, family na Taifa.
Rai hiyo imetolewa na  Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt Faustine Ndugulile Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga wakati wa uzinduzi wa klabu za wasichana katika shule ya Sekondari ya Mwendakulima.

Dkt. Ndugulile amesema kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia vinazidi kushamiri katika jamii zetu hususan katika meneo ambayo bado wanafuata mila na desturi ambazo zinamkandamiza mtoto wa kike na mwanamke.

Ameongeza kuwa namna bora ya kupambana na ukatili wa kijinsia ni kwa watoto wa kike kutonyamaza pale ambapo wanafanyiwa vitendo vya ukatili hasa kuozeshwa na kushawishiwa kuingia kwenye mahusiano ya kingono katika umri mdogo: mambo yanayosababisha mimba na ndoa za utotoni.

“Kila mtu aunge mkono juhudi zetu za pamoja za kutokomeza mimba na ndoa za utotoni kwa kuacha usiri na kushirikiana kutoa taarifa ya vitendo vya ukatili wa kijinsia  kwa mamlaka zilizopo“ alisiistiza Dkt. Ndugulile.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Fadhili Nkulu amesema kuwa Wilaya yake inaendelea kushirikiana na jamii na wadau wa maendeleo katika kuendeleza juhudi za Serikali za Kupambana na Vitendo vya Ukatili wa Kijinsia zikiwemo mimba na ndoa za utotoni ili kuwapatia watoto wa kike haki yao ya kuendelezwa na kuwaandaa kuwa nguvu kazi bora ya Taifa la uchumi wa kati na wa viwanda.

Naye mmoja wa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mwendakulima Mwajuma Salum amesema klabu za wasichana zinawasaidia sana watoto wa kike kujitambua kwa kupata elimu zinazowawezesha kupamabana na vitendo vya ukatili wa kijinsia hasa mimba na ndoa za utotoni. 

Aidha, ameeleza kuwa mbinu wanazopata zinawasaidia kuishi na wanafunzi wenzao wa kiume kama kaka na dada wakiwa na jukumu la kuwalinda na kuwapa kuwashauri kuzingatia wajibu wao katika masomo.

No comments:

Post a Comment