Wednesday 2 May 2018

MGODI WA GGM KUZINDUA MBIO ZA KILI CHALLENGE KWA MWAKA 2018 JIJINI DSM


Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kwa kushirikiana na Tume ya kuthibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) inatarajia kuzindua zoezi la upandaji wa mlima Kilimanjaro (Kilimanjaro Challenge 2018),  na kuendesha harambee ya kuchangisha fedha kwa mwaka 2018 kwa ajili ya afua za UKIMWI nchini. 
Shughuli hii inatarajiwa kufanyika tarehe 4 Mei 2018 mwaka huu katika Hoteli ya Hyatt Regency Kilimanjaro iliyopo jijini Dar es Salaam.

Mgeni rasmi katika uzinduzi huo anatarajiwa kuwa Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa ambapo atafanya zozezi la ugawaji wa fedha zilizokusanywa mwaka jana 2017 zilizopatikana baada ya wadau mbalimbali kupanda na  kuendesha baiskeli kwa kuzunguzuka Mlima Kilimanjaro .

Kilimanjaro Challenge against HIV & AIDS ni mfuko unaochangia juhudi za serikali  katika mapambano dhidi ya UKIMWI na kutoa elimu kwa jamii kuhusu maambukizi ya Virusi Vya UKIMWI (VVU).

Kilimanjaro Challenge ni mfuko muhimu unaoshirikiana na taasisi za nje na ndani ya nchi katika kuendeleza mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI kwa jamii ya Kitanzania na Dunia kwa ujumla ili kuwapa matumaini ya kuhakikisha jamii inabaki bila kuathiriwa na VVU/UKIMWI katika miaka ijayo.

Mfuko huo pia unalenga kuisaidia Serikali kukabiliana na VVU//UKIMWI sambamba na kutoa nafasi kwa watalii wa ndani na nje kuupanda mlima Kilimanjaro.

Takwimu zilizotolewa na Tume ya Kuthibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS), zimeonesha kupungua kwa maambukizi ya virusi vya UKIMWI kutoka asilimia 5.1 %  mwaka 2011/ 2012 hadi asilimia 4.7% mwaka 2016/17.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS, Dkt. Leonard Maboko anasema, “ Mwaka wa 2016, inakadiriwa kuwa watu milioni 1.5 nchini wanaoishi na VVU na UKIMWI hadi sasa  watu 225
 wanapata maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa siku. 

"Ugonjwa huu umewaathiri zaidi vijana na watoto yatima zaidi. Tunahitaji kubadilisha hali hii. Lengo la kukusanya fedha ni kuweza kusaidia serikali ya Tanzania katika jitihada zake kufikia sifuri tatu. 

"Sifuri katika maambukizi mapya, sifuri ya unyanyapaa, sifuri katika vifo vitokanavyo na UKIMWI. TACAIDS kwa kushirikiana na Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) na wadau wengine kwa kupitia mpango huu wa Kili Challenge tunapenda kutoa mchango na ushirikiano wetu kwa Taifa ili kutunisha mfuko utakaowezesha kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa huu. 

"Tuna matumaini ya kujenga timu imara yenye hamasa ya kupambana na janga hili. Tunatoa wito kwa makampuni na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, wajitokeze ili tusaidiaane kutunisha mfuko wa Kili Challenge na mwishowe kufikia malengo yetu ya kuhakikisha tunakuwa na kizazi kisicho na maambukizi ya VVU/ UKIMWI,” Alisema Dkt. Leonard Maboko.

“Watoto watakaoshiriki katika zoezi la Kilimanjaro Challenge mwaka huu ni wa kiume na wa kike wenye umri kuanzia miaka 13. Watoto hao yatima kutokana na tatizo la VVU/ UKIMWI wamesaidiwa na Kituo cha kulea watoto yatima cha Moyo wa Huruma Orphanage Center kilichopo Geita.

"Changamoto kubwa inayotokana na janga hili ni pamoja na maelfu ya watoto yatima wanaohitaji misaada baada ya wazazi wao kufariki, wajane wasiokuwa na kipato, pamoja na wazee wanaolazimika kuwalea wajukuu walioachwa na watoto wao ambao walifariki kutokana kwa ugonjwa huo."


No comments:

Post a Comment