Friday 28 July 2017

GHARAMA YA CHANJO YA HOMA YA INI IMEPUNGUA



Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee  na Watoto Ummy Mwalimu
Bohari Kuu ya Dawa (MSD) imepunguza gharama ya chanjo ya ugonjwa wa homa ya ini kutoka shilingi 22,000 kufikia shilingi 5,300 ili kusaidia upatikanaji wa chanjo hiyo katika vituo vingi vya tiba hapa nchini hususani vituo vya Umma.

Hayo yamesemwa leo  Jijini Dar es Salaam  na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee  na Watoto Ummy Mwalimu  katika maadhimisho ya siku ya homa ini Duniani  yanayoadhimishwa kila mwaka Julai 28 kama ilivyopendekezwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) Kwa lengo la kuelimisha jamii  na kutambua athari za ugonjwa huo.

Ummy amesema kuwa Serikali imeamua kununua dawa ya chanjo ya ugonjwa huo moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji ili kuwawezesha Wananchi kuipata kwa gharama nafuu zaidi  kwa lengo la kuunga mkono kauli mbiu ya maadhimisho ya ugonjwa huo kwa mwaka huu ambayo inasema “Tokomeza Homa ya Ini (Eliminate Hepatitis)”.

“Matibabu ya homa ya ini yana gharama kubwa, ambapo kwa mgonjwa aliyepata maambukizi ya virusi C anaweza kutibiwa kwa millioni tatu hadi tano kulingana na muda wa tiba ndio maana tunasema bora kinga kuliko tiba,” alisema Ummy.

Aliongeza kuwa  chanjo inayotolewa nchini  kwa sasa ni  ya  virusi B inayojulikana kama Hepatitis B  japo chanjo ya virusi A ipo na inatolewa nchi nyingine  kutokana na Tanzania kukabiliwa  na  aina mbili tu virusi ambavyo  ni virusi B na C. 

“Kwa sasa hakuna ushahidi wa mlipuko wa homa ya Ini nchini, hata hivyo wananchi wa Tanzania na Afrika Mashariki wapo katika hatari ya kupata ugonjwa huu kutokana na njia za maambukizi kufanana kwa kiasi na zile za maambukizi ya virusi vya ukimwi,” aliongeza Ummy.

Waziri huyo  alisema kuwa chanjo hiyo ilianza kutolewa bure nchini kwa watoto waliozaliwa kuanzia mwaka 2003 na kuendelea. Aidha mwaka 2015 zaidi ya dozi 650,000 ilitolewa kwa watumishi wa afya ili kuwakinga na hatari ya  maambukizi  ya ugonjwa huo wakati wakitekeleza majukumu yao ya utoaji huduma kwa waathirika wa ugonjwa huo.

“Kwa sasa tunaangalia ni namna gani tunaweza kuifikia jamii iliyobaki ili tuweze kuwapatia chanjo, Serikali imeshafanya mchanganuo rasmi ambao umeonyesha kiasi cha gharama ya chanjo, vitendanishi vya vipimo vya awali, kutunza chanjo, kusambaza chanjo na shughuli yenyewe ya uchanjaji,” alifafanua Ummy.

Aidha amesema kuwa kwa sasa chanjo hiyo inatolewa kwa malipo ya shillingi 50,000 mpaka 70,000 kwa dozi moja  katika baadhi ya vituo binafsi vya Afya  ikiwa  ni pamoja na Premier Care Clinic, IST Na Hindu Mandal kwa mkoa wa Dar es Salaam. 


Ummy amewataka wananchi kujiepusha na maambukizi ya ugonjwa huo kwa kuachana na matumizi ya dawa kiholela, vilevi kupita kiasi, madawa ya kulevya, matumizi ya sindano zisizo salama na vihatarishi vyote vya maambukizi ya ukimwi kwani wagonjwa wa ukimwi wapo kwenye hatari kubwa ya kupata maambukizi kuliko wazima.

No comments:

Post a Comment