Tuesday 29 August 2017

SERIKALI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA SEKTA BINAFSI KUFANIKISHA TANZANIA YA VIWANDA





Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango amesema serikali inathamini mchango wa sekta binafsi na itaendelea kushirikiana nayo katika kuhakikisha azma ya Tanzania ya viwanda inafikiwa.
Dkt. Mpango alisema hayo Jijini Dar es Salaam leo alipokuwa akizindua kitabu cha Safari ya Tanzania kuelekea katika Uchumi wa Viwanda 2016- 2056, kilichoandikwa na watanzania wazalendo Bw. Ali Mufuruki, Gilman Kasiga na Moremi Marwa.

‘’Kitabu hiki ni kama mkombozi kwa sisi watunga sera kwani kitatusaidia katika kuyafanyia kazi mapendekezo ambayo yametolewa ili kuhakikisha Tanzania ya viwanda inawezekana, nimewaelekeza pia Tume ya Mipango na Idara ya sera katika Wizara ya Fedha kuchukua mapendekezo ambayo wataona yataisaidia serikali katika kutekeleza azma yake ya kuendeleza viwanda’’alisema Dkt. Mpango

Bw. Ali Mufuruki mmoja wa watunzi wa kitabu hicho alisema wameamua kuunganisha mawazo yao pamoja na kutumia utaalamu na uzoefu wao katika masuala mbalimbali ya maendeleo na uchumi ili kuisaidia serikali kuweza kuondokana na uchumi unaotegemea kilimo na hatimaye kuwa nchi ya viwanda.

‘’Kuna changamoto nyingi zinazozikabili nchi zinazoendelea ikiwemo ukosefu wa utaalamu katika kilimo cha kisasa, ukosefu wa mitaji pamoja na kutokuwa na teknolojia ya kutosha hivyo kwa kuwa azma ya Mh. Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni kuwa na nchi ya uchumi wa kati unaotegemea viwanda, tukaona tumuunge mkono katika kutimiza ndoto hiyo kwa kuandika kitabu hiki’’ alisema Mufuruki.

Bw. Mufuruki alisema kuna mambo mengi mazuri ya kulisaidia taifa ambayo yameainishwa katika kitabu hicho hivyo ni vyema watanzania wa kawaida, wasomi, wachumi na hata wawekezaji wakakisoma ili kuona kila mmoja katika nafasi yake anawezaje kuisaidia nchi kutoka hapa ilipo na kufikia katika malengo iliyojiwekea.

Kwa upande wake Bw.Gilman Kasiga ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya General Electric katika ukanda wa Afrika Mashariki, alisema ni vyema Tanzania ikawekeza katika masomo kwa kutambua vipaumbele kama inavyofanya nchi ya Ujerumani ambapo sio kila anayesoma ni lazima afikie ngazi ya shahada ndipo aonekane anaweza kuleta mchango katika maendeleo.

Bw. Kasiga alisema asilimia 70 ya wanaomaliza shule hapa nchini wanakimbilia kusoma shahada na kusahau kwamba kuna masomo mengine katika ngazi za astashahada na cheti ambayo kama yakifundishwa kwa umakini na kwa kuzingatia fani husika yanaweza kuzalisha wataalamu wengi ambao wataisaidia nchi kupiga hatua kimaendeleo na pia wao kupata ajira kwa urahisi katika viwanda.


Alisema elimu ya vyuo vikuu ni ya kuandaa wasimamizi yaani mameneja na sio watendaji au wafanya kazi na mafundi hivyo ameshauri mitaala ya vyuo iendane na ukuaji wa viwanda ili wataaalamu hao waweze kutumia taaluma zao katika kulitumikia taifa.



No comments:

Post a Comment