Thursday 15 December 2016

DALADALA DODOMA ZAGOMA KUPINGA MANYANYASO



Zaidi ya mabasi 70 ya daladala yanayosafirisha abiria katika baadhi ya njia za manispaa ya Dodoma, yamegoma kutoa huduma kwa siku nzima ya leo kutokana na madai ya kunyanyaswa na askari wa usalama barabarani.
Daladala hizo zinazotoa huduma kati ya Jamatini na Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) pamoja na Jamatini na Veyula, zilisimamisha huduma zake kwa siku nzima ya leo zikipinga manyanyaso ya askari hao.

Baadhi ya madereva wa mabasi hayo, wamesema wamechoshwa na manyanyaso kutoka kwa askari hao kwa vitendo vyao vya kuwakamata kiuonevu.

Wamesema sababu kubwa ya mgomo wao ni rushwa na manyanyaso wanayofanyiwa na baadhi ya askari hao wa usalama barabarani.

Hata hivyo, akijibu malalamiko ya madereva hao, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Dodoma, Marisone Mwakyoma, amesema sheria zipo wazi kama kuna mtu anaombwa rushwa na kutoa, wote wana makosa kwa sababu zipo ngazi za kuripoti matukio hayo.


Afisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) mkoa wa Dodoma, Conrad Shio, amesema baada ya kutokea kwa mgomo huo waliweza kutoa kibali kwa magari mengine kuweza kubeba abiria wasipate shida ya usafiri.

No comments:

Post a Comment