Tuesday 8 November 2016

SERIKALI YAZITAKA TAASISI ZA HAKI ZA BINADAMU AFRIKA MASHARIKI KUTOA ELIMU KWA UMMA KUTATUA MIGOGORO

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome
Serikali imezitaka taasisi zinazosimamia mtandao wa haki za binadamu katika nchi za Afrika Mashariki kupanua wigo wa utoaji elimu kwa umma, hatua inayolenga kutatua migogoro ya mara kwa mara inayojitokeza katika jamii.

Wito huo umetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome, wakati alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa taasisi zinazosimamia Haki za Binadamu katika nchi za Afrika Mashariki.

Prof. Mchome alisema jukumu la ulinzi na usimamizi wa haki za binadamu katika eneo la jumuiya hiyo ni la kila nchi mwanachama, kwa kuwa msingi wa maendeleo wa nchi yoyote duniani hupatikana katika sehemu yenye hali ya utulivu na maeleweno.

Kwa mujibu wa Prof. Mchome alisema kuanzia mwezi Mei hadi Septemba mwaka huu, nchi zote za Afika Mashariki ziliwasilisha taarifa zao kuhusu hali ya haki ya kibinadamu katika mataifa yao, mjini Gevena Uswisi, ambapo ripoti hizo zitatumika katika kujadili changamoto zilizojitokeza na hatua za kuchuliwa katika kuboresha.

Aidha Prof. Mchome alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizopiga hatua kubwa katika kuimarisha haki za kibinadamu duniani ingawa yapo maeneo kadhaa yenye migogoro  ikiwemo migogoro ya wakulima na wafugaji, ingawa Serikali imechukua hatua za makusudi  za kukabiliana na hali hiyo.

“Serikali imekuwa ikipeleka  taarifa Bungeni kuhusu migogoro ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji, na maamuzi ya kisera yanayofanywa na Serikali, pamoja na kuendelea kuelimisha umma  kuhusu masuala ya sheria mkononi.” Alisema Prof. Mchome.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (CHRAG), Mary Massay alisema suala la haki za binadamu ni dhana mtambuka kwa kuwa inagusa sekta muhimu za maisha ya binadamu ikiwemo elimu, maji, ardhi, maliasili na kadhalika.

Alisema mkutano huo umeandaliwa makhususi kwa ajili ya kupokea na kujadili taarifa ya ripoti za utafiti kuhusu hali ya haki za binadamu katika nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Tanzania.

Alisema utafiti huo umejikita zaidi katika kubaini viashiriia vya uvunjifu wa haki za baindamu katika nchi hizo na hatua zinazopaswa kuchuliwa na Serikali za nchi wanachama  ili kuzuia machafuko katika siku za usoni kutokana uzoefu uliojitokeza katika nchi za Rwanda na Burundi.

Kwa mujibu wa Massay alisema migogoro mingi inayotokeza katika nchi nyingi za Afrika hususani zilizopo katika ukanda wa Afrika mashariki husababishwa na kauli na matamko ya viongozi kuagiza jambo ambalo linakwenda kinyume na matakwa ya wananchi walio wengi.

Naye Naibu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu ya nchini Kenya, George Morara alisema hali ya haki za kibinadamu ya nchi hiyo ni ya kurithisha ingawa mamlaka za dola katika nchi hiyo zimekuwa zikikuwa zikitumia nguvu kubwa kuthibiti raia kwa kutumia sheria zilizopo.


Alisema miongoni mwa sheria ni sheria ya kimataifa inayohusu haki za kiraia na kisiasa ambapo, baadhi ya maafisa usalama nchini humo wamekuwa wakitumia nguvu kuzuia mikusanyiko ya kisiasa kwa kigezo cha kudhibiti matukio ya kigaidi nchini humo.

No comments:

Post a Comment