Thursday 2 November 2017

M/KITI WA KIJIJI CHA KIFUFU KATA YA BUGALAMA MKOANI GEITA ATENGWA NA WANAKIJIJI KWA KUGOMA KULIPA FAINI

Mwenyekiti wa kitongoji cha Mwabalogi Kijiji cha Kifufu ambaye ambaye ametengwa na wananchi kutokana na kugoma kulipa faini ya shilingi laki sita.

Diwani wa kata ya Bugalama , Luponya Masalu  akiwasisitiza wananchi kuishi kwa amani na kusameheana makosa yao ili kuruhusu maendeleo kwenye Kijiji cha Kifufu.
Baadhi ya wananchi wakimsikiliza Diwani wakati alipokuwa akihutubia hadhara hiyo.

Wakina Mama wakifuatilia Mkutano huo.

Meza kuu ikiongozwa na Mwenyekiti pamoja na wajumbe wa kikao hicho.
     
Wananchi wa Kijiji cha Kifufu Kata ya Bugalama Wilayani Geita wameazimia kumtoza faini ya shilingi laki sita  Mwenyekiti wa kitongoji cha Mwabalogi kutokana na kuwepo kwa tabia ya watoto wake kuingia kwenye makazi ya wanakijiji na kuiba mifugo pamoja na mazao.

Hata hivyo mwenyekiti huyo Bw Nchemba Kasomeko amesababisha hali ya sintofahamu kwa wanakijiji baada ya kugoma kuomba msamaha na kukiri makosa ambayo yamesababishwa na watoto wake mbele ya mkutano wa hadhara ulioitishwa na diwani wa kata hiyo uliokuwa na lengo la kuleta suluhu baina yake na wanakijiji kutokana na tuhuma za kuwahifadhi wahalifu wakiwemo wajukuu zake jambo ambalo limesababisha uvunjifu wa sheria.

Katika Mkutano huo Bw Nchemba anadaiwa kuwakejeli wananchi pamoja na viongozi wa kata wakiongozwa na Mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya kata hiyo baada ya kumtaka alipe faini ya Sh Laki 6 ya kuhifadhi wahalifu baada ya wajukuu zake kutuhumiwa kwa wizi wa matikiti maji kwenye shamba la Leonard Martin kwa kuwaita masikini.

“Ndugu zanguni mimi nashangaa watu kusongamana kila wakati mnanitafuta mimi tu,nimekuwa kama dume la wizi na nyie viongozi hapa mbele ni wanafiki tu na kitu cha kukaa ninasumbuliwa nitoe laki sita wakati sio mwizi  wizi ni watoto mliwaachia nyie kuwa mmewasamehee leo tena mnataka nitoe mahela mengi wanakijiji nilishawai kufika  kwako nikakomba mboga tatizo umasikini wenu unawasumbua au mnataka nitoke humu nijenge Geita”Alifoka kwenye Mkutano huo.

Kutokana na Majibu ya Nchemba kuwa ya kejeli na kuto kuafiki kulipa faini ya Sh Laki 6, baadhi ya wananchi wamechukizwa na kauli zake na kuuomba uongozi wa kijiji na kata kuondoka nae .

Kweli Nchemba asijione anavyo sana kuliko wananchi kama kuna faini naomba atoe hiyo faini sio yeye ajifanye anavyo sana jamani kwani Mungu aliumba Masikini na matajiri” Alisema Getruda Kachwele.

“Ndugu mwenyekiti nadhani Muda unakwenda na hili la Nchemba hatutalimaliza sisi tulikwisha wapatia mtu wenu mnaonaje kama mtamchukua muende nae tu maana sisi huyu hatuwezi kuendelea kuwa na mtu wa namna hii kijijini hapa” Alisikika akisema Musa Msafiri.

Kufuatia madai hayo kwa wananchi Diwani wa kata Hiyo, Luponya Masalu amemtaka Bw Nchemba kuwaomba radhi wananchi na kuwalipa wananchi pesa ya faini ambayo anadaiwa lakini amekaidi na kumtaka diwani kumuacha akajifikirie.


Julai 23 Mwaka huu Mkutano Mkuu wa Kijiji hicho uliketi na kuazimia Bw, Nchemba alipe kiasi hicho cha fedha ambapo alikubali lakini leo ameyatupilia mbali maamuzi hayo .

No comments:

Post a Comment